Breaking News

YANGA KIBARUANI TENA KUIKABILI ST LOUIS YA SHELISHELI


WAWAKILISHI wa Tanzania kwenye michuano ya ligi ya mabingwa Afrika, Yanga leo ina kibarua kigumu mbele ya St Louis ya Shelisheli kwenye mchezo wa marudiano wa michuano hiyo hatua ya awali.

Yanga inawakabili wapinzani wao hao huku wakiwa mbele kwa bao 1-0 kufuatia ushindi walioupata kwenye mchezo wa kwanza jijini Dar es Salaam.

Kocha msaidizi wa Yanga, George Lwandamina, aliiambia Nipashe kutoka Shelisheli kuwa mchezo huo wa leo hautakuwa rahisi lakini wamejipanga na kuwashukia kivingine wapinzani wao hao.

"Tunahitaji ushindi, ndio kitu pekee tulichokifuata huku, hautakuwa mchezo mwepesi kwa sababu kwa namna nilivyowaona wapinzani wetu, si timu ya kuidharau," alisema Lwandamina.

Alisema watajitahidi kucheza soka la kasi ndani ya dakika 20 za kwanza kujaribu kutafuta bao la kuongoza hili kuwapa presha wapinzani wao hao.

Yanga leo haitakuwa na mshambuliaji wake nyota, Obbrey Chirwa, lakini itawategemea nyota wengine, Ibrahim Ajibu na Papy Tshishimbi kuzamisha  jahazi la St Louis.

Meneja wa timu hiyo, Hafidh Saleh, aliambia Nipashe kutoka nchini humo kuwa wachezaji wote walioongozana na timu wapo katika hali nzuri.

Ili kusonga mbele, Yanga inahitaji ushindi wa aina yoyote au sare kwenye mchezo huo wa leo.

Kwenye mchezo wa kwanza kwenye uwanja wa taifa, goli pekee la Yanga lilifungwa na kiungo Juma Mahadhi huku pia mashabiki wakishuhudia Chirwa akikosa penalti. 

No comments