Breaking News

Meya wa Mwanza aomba kukutana na Rais kwa siri

Meya wa Jiji la Mwanza, James Bwire

Tangu Aprili, Bwire na Mkurugenzi wa Jiji la Mwanza, Kiomoni Kibamba wamekuwa katika mgogoro.

Mwanza. Meya wa Jiji la Mwanza, James Bwire ameomba kukutana na Rais John Magufuli kwa siri kwa kuwa kuna mambo ambayo hawezi kuyasema hadharani.

Bwire ametoa ombi hilo leo Jumanne Oktoba 31,2017 mbele ya Rais Magufuli baada ya kutambulishwa na Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, John Mongella wakati wa hafla ya uzinduzi wa kiwanda cha bidhaa za plastiki cha Victoria Moulders Ltd eneo la Igogo wilayani Nyamagana.  

Meya Bwire jana Jumatatu Oktoba 30,2017 alikamatwa na kufikishwa Kituo Kikuu cha Polisi jijini Mwanza wakati wa mapokezi ya Rais Magufuli katika Uwanja wa Ndege wa Mwanza.

Kuachiwa kwa meya huyo kulitangazwa baadaye na Rais alipohutubia mkutano wa hadhara eneo la Nyakato.

Rais Magufuli alitoa kauli hiyo alipowaeleza wananchi kuwa mabango waliyokuwa wamebeba ameyaona likiwemo lililoeleza kuwa Meya Bwire anashikiliwa na Polisi.

Awali, ilielezwa Bwire alishikiliwa Kituo Kikuu cha Polisi kwa amri ya mkuu wa mkoa, Mongella.

Hata hivyo, Mongella akizungumza naMwananchi, alikana kutoa agizo kwamba meya huyo akamatwe.

Akizungumzia hilo, Mariam Lima ambaye ni katibu wa mitandao ya taasisi ya Alliance inayomilikiwa na meya Bwire alisema kuwekwa kwake ndani kulitokana na agizo la mkuu wa mkoa.

Tangu Aprili, Bwire na Mkurugenzi wa Jiji la Mwanza, Kiomoni Kibamba wamekuwa katika mgogoro kila upande ukiutuhumu mwingine kuhujumu shughuli za maendeleo

No comments