Watoto pacha wa Morogoro kutenganishwa
Daktari Bingwa wa Upasuaji wa Watoto, Zaituni Bokhari (Kushoto) akielezea namna ambavyo wametoa matibabu kwa watoto pacha walioungana. Dk Bokhari ambaye pia ni bingwa aliyebobea upasuaji wa watoto Afrika Mashariki amesema wanatarajia kuwatenganisha baadaye mwaka huu. Picha na Erick Boniphace
Pamoja na mambo mengine Dk Bokhari amesema vipimo vya damu vimeonyesha kuwa kila mtoto ana mfumo wake na kwamba hakuna hitilafu yoyote itakayokwamisha zoezi hilo.
Dar es Salaam. Daktari Bingwa wa Upasuaji wa Watoto Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH), Zaituni Bokhari amesema baada ya vipimo imegundulika kuna uwezekano wa kuwatenganisha watoto pacha walioungana.
Dk Bokhari ambaye amebobea katika upasuaji huo Afrika Mashariki, ameyasema hayo leo asubuhi alipokuwa akitoa majibu ya vipimo vilivyochukuliwa hospitalini hapo kwa takribani wiki nzima.
"Vipimo vya damu vimeonyesha kila mtoto ana mfumo wake na hawana maambukizi ya aina yoyote, ugumu unakuja kwenye ini na moyo ambapo wanategemeana ila uwezekano wa kutenganishwa upo,"amesema Dk Bokhari.
Majibu hayo yamekuja siku chache baada ya pacha hao kupimwa vipimo vya radiolojia ikiwemo CT Scan, MRI, X Ray kipimo cha moyo (ECO) pamoja na vipimo vyote vya damu.
Watoto hao waliozaliwa katika hospitali ya Misheni ya Berega iliyopo Kanda ya Mashariki mkoani Morogoro, Julai 21 mwaka huu wamenaza kuchukuliwa vipimo mbalimbali vya awali.
No comments