Breaking News

Mashtaka mengine 6 waliyoongezewa Rugemarila na Harbinder Seth haya hapa

Mfanyabiashara maarufu James Rugemarila na mmiliki wa mitambo ya kufua umeme ya IPTL, Harbinder Seth wamefikishwa mbele ya Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu wakikabiliwa na mashtaka 12, badala ya mashtaka sita waliyosomewa awali.

Kwa mujibu wa Wakili wa Serikali Mwandamizi,Shedrack Kimaro aliyesoma Mashtaka kwa Hakimu Mkazi Mkuu, Huruma Shaidi, mashtaka hayo ni:

1: Kutakatisha fedha Dollar 22,198,544.60 na Tsh 309,461,300.27

Kati ya November 29, 2013 na January 23, 2014 maeneo tofauti ya Dar es Salaam washtakiwa kwa pamoja walitenda kosa la kutakatisha fedha wakichukua fedha kutoka BoT Dollar 22,198,544.60 na Tsh 309,461,300.27 wakati wakijua fedha hizo ni zao la kujihusisha na genge la uhalifu.

2: Kutakatisha fedha Dollar 22,198,544.60

Aidha, katika Shtaka la pili kati ya sita yaliyoongezwa, Kimaro alidai kuwa November 29, 2013 katika tawi la kati la Benji ya Stanbic Tanzania wilaya ya Kinondoni Sethi alitakatisha fedha kwa kuchukua BoT Dollar 22,198,544.60 wakati akijua fedha hizo zimetokana na zao la kujihusisha na genge la uhalifu.

3: Kutakatisha fedha Tsh. 309,461,300,158.27

Kwa upande wa Tatu, Sethi anadaiwa kuwa kati ya November 29, 2013 na March 14, 2014 katika tawi la kati la Benji ya Stanbic Kinondoni Dar es Salaam alitakatisha fedha, Tsh. 309,461,300,158.27 kutoka BoT wakati akijua fedha hizo zimetokana na zao la kujihusisha na genge la uhalifu.

4: Kutakatisha fedha Tsh. 73,573, 500,000

Shtaka ya Nne, inadaiwa January 23, 2014 katika Benki ya Mkombozi tawi la St Joseph Cathedral, Rugemarila alitakatisha fedha, Tsh. 73,573, 500,000 kutoka kwa Seth wakati akijua fedha hizo zimetokana na zao la kujihusisha na genge la uhalifu.

5: Kutakatisha fedha Dollar 22,000,000

Pia shtaka la Tano, Kimaro alidai kuwa January 23, 2014 katika benki ya Mkombozi tawi la St Joseph Cathedral, Rugemarila alitakatisha fedha Dollar za Marekani 22,000,000 kutoka kwa Seth wakati akijua fedha hizo ni zao la uhalifu.

6: Kuhamisha fedha Rand (zar 1,305,800)

Shtaka la Sita, Seth anadaiwa kuwa January 28, 2014 katika tawi la kati la Benki ya Stanbic wilaya ya Kinondoni alihamisha Rand (zar 1,305,800 kwenda kwenye akaunti namba 022655123 katika Standard bank Land Rover Sandton Johannesburg wakati akijua katika kipindi anahamisha fedha hizo zimetokana na zao la kujihusha na genge la uhalifu.

Hata hivyo, washtakiwa hawakuruhusiwa kuongea chochote kwa sababu Mahakama ya Kisutu haina mamlaka ya kusikiliza ambapo baada ya kusomewa mashtaka hayo, Wakili Kimaro alidai upelelezi bado haujakamilika na washtakiwa wamepelekwa rumande hadi July 14, 2017.

No comments