Breaking News

Askari wanne wafuzu mafunzo ya uokozi baharini

JESHI  la Zimamoto na Uokoaji nchini limefanikiwa kupata wataalamu wa maokozi ya majini waliopatiwa mafunzo na wataalamu wa maokozi ya baharini kutoka nchini Ujerumani.

Akizungumza wakati wa kufunga mafunzo hayo maalum ya uzamiaji  majini na maokozi ya baharini katika Visiwa vya Bongoyo jijini Dar es Salaam Kamishina wa Oparesheni wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji, Billy Mwakatage, amesema jumla ya askari wanne wamefuzu mafunzo hayo na kutunukiwa vyeti vya kimataifa kwa ajili ya maokozi ya majini hivyo kuongeza idadi ya wataalamu hao kufikia saba.

“Lengo la mafunzo haya ni kuwajengea uwezo askari ili waweze kumudu majukumu yao kwa ufanisi na hali ya juu,” alisema.

Kwa upande wake mkuu wa kitengo cha maokozi, Mrakibu Msaidizi, Bashiri Madhehebi amesema kufuzu kwa askari hao wanne kunaifanya Tanzania kuwa ni moja ya nchini zenye uwezo wa kufanya maokozi ya baharini na kuongeza usalama kwenye usafiri wa majini.

Naye mkufunzi  wa mafunzo ya uokoaji kutoka taasisi ya SES iliyopo nchini Ujerumani aliyesimamia mafunzo hayo, Bjon Schenkel amesema wataendelea kushirikiana na Tanzania katika kufundisha wataalamu wa maokozi ya baharini katika kuimarisha uhusiano baina ya nchini hizo mbili.

Aidha kwa upande wake, Mrakibu Msaidizi, Athumani Nassa ambaye ni mkuu wa mafunzo wa jeshi hilo, amesema wanakabiliwa na changamoto ya ukosefu wa miundombinu kama ‘swimming pool’ na kusababisha kuomba kwa wadau, jambo linalosababisha kuwa na idadi ndogo ya wahitimu.

No comments