Breaking News

TRA yaeleza sababu za kusitisha utoaji wa leseni za udereva


Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) imeeleza kuwa itaendelea na zoezi la utoaji wa leseni za udereva kwa wote walioomba, baada ya zoezi hilo kusitishwa kwa muda.

Mkurugenzi wa Elimu na Huduma kwa mlipa kodi, Richard Kayombo, ameeleza kuwa zoezi hilo litaanza tena kuanzia wiki ijayo.

Kayombo alisema kuwa upungufu wa malighafi ndiyo kimekuwa chanzo cha usitishwaji wa zoezi hilo ila kwa sasa tayari wameshapata malighafi za kutosha kuwawezesha kuendelea na zoezi.

“Kulikuwa na uhaba wa malighafi ndiyo maana tukashindwa kuchapisha leseni mpya za udereva. japo kwa sasa tayari tumeshanunua malighafi ya kutosha na tutaanza kuchapisha leseni kuanzia wiki ijayo,” alisema Kayombo.

“Madereva walioomba kupatiwa leseni watazipata ndani ya wiki moja. tumejipanga kuhakikisha kuwa madereva wote walioomba leseni, hasa wanaoendesha magari ya huduma kwa umma, wanapata leseni zao ndani ya muda mfupi ili waendelee kutoa huduma kwa jamii,” aliongeza.

Kumekuwapo na malalamiko mengi kutoka kwa wananchi wa maeneo mbalimbali hapa nchini kuhusiana na ucheleweshwaji wa upatikanaji wa leseni za udereva, huku wengine wakilalamika kutozwa faini na askari wa kikosi cha usalama barabarani kwa kuwa leseni walizo nazo zimekwisha muda wake wa matumizi.

No comments