Breaking News

Ndoa ya Zamaradi Mketema yazua gumzo

Zamaradi asema alhamdulilah akimaanisha namshukuru Mungu

Dar es Salaam. Ndoa ya mtangazaji wa kipindi cha Take One kinachorushwa na kituo cha televisheni cha Clouds, Zamaradi Mketema imezua mijadala mtandaoni, huku wengi wakihoji iwapo ni kazi mpya ya sanaa ya mwandaaji huyo wa filamu ya Kigodoro.

Hata hivyo, taarifa zilizosambaa mtandaoni tangu usiku wa kuamkia leo Jumamosi zinaeleza mtangazaji huyo ameolewa na ndugu wa karibu wa kiongozi katika Serikali ya Awamu ya Tano.

Zamaradi kupitia ukurasa wake wa Instagram ameweka picha ya harusi yake, huku sura ya bwana harusi ikiwa haionekani vizuri na kuandika 'Alhamdulilah'.

Katika mitandao baadhi ya watu wamepongeza mtangazaji huyo huku wengine wakionyesha kushangazwa na tukio hilo kwa madai kuwa limekuwa ni la muda mfupi.

Rafiki wa karibu wa mwanadada huyo, Faiza Ally amempongeza kupitia ukurasa wake wa Istagram kwa kuandikia, “Ndoa yako iwe ya kheri Inshaallah.”

Mwingine aliyetuma ujumbe ni Jumalokole2 aliyeandika kupitia ukurasa wake wa Istagram akisema, “Wanawake wote mnapaswa kumuiga @zamaradimketema nimependa sana sema nyie mwalimu wenu......mwenzenu katumia fursa ..kaacha mbili kaifuata 6.”

Baadhi ya wasanii nchini wamempongeza kupitia mitandao ya kijamii. Msanii wa filamu Johari Chagula ameandika kwenye mtandao wa Instagram akisema, “Hongera sana Zama Mungu akuongeze vyema katika maisha mapya hakuna kitu kizuri kama amani ya nafsi furaha ya moyo, hakika hakuna kinachoshindikana chini ya jua, Nina hakika nitafuata nyuma.”

No comments