Breaking News

Miguu ya Ajib inavyopishana na akili ya Niyonzima

Abdul Dunia

Titi la mama ni tamu. Hata likiwa la mbwa. Kiswahili naazimu. Sifayo inayofumbwa. Niimbe ilivyo kubwa. Toka kama chemchem. Titi la mama litamu jingine haliishi hamu. Aliwahi kuandika hayati Shaaban Robert katika moja ya vitabu vyake.

Shaban Robert ni kati ya waandishi walitokea kunivutia kutokana na kalamu yake anapoitumia. Hakuna kama Shaaban Robert. Acha niishie kusema hivyo. Hebu jaribu kufikiria maneno hayo ya nguli huyo katika kalamu kwa utulivu kama unashuhudia ile filamu ya uchaguzi wa Yanga mwaka jana.

Manji anachukua fomu, Msumi anasakwa na wanachama. Unavuta pumzi kisha unaendelea kufikiria. Manji anashinda, Mzee Akilimali anampongeza. Hakika ilikuwa filamu isiyoisha hamu.

Baada ya uchovu niliokuwa nao, nimeamua kuchukua kaseti mbili za Simba na Yanga kwa ajili ya kutazama. Moja kwenye mechi kati ya Simba na Mbeya City na nyingine Yanga na Ruvu Shooting. Zote za msimu uliopita.

Nimetazama kaseti hizo na nimezielewa. Nimeona wachezaji wawili tu. Kwanza nimemuona Ibrahim Ajib alafu nimemalizia kumuona Haruna Niyonzima maarufu kama Fabregas. Hao tu ndio niliowaona katika mechi hizo.

Kufananishwa na mchezaji kama Fabregas sio jambo la kawaida kabisa. Lazima uwe na kitu cha ziada ili kweli ufananishwe naye. Si mlimuona yule Idd maarufu kama Ronaldo wa Misosi FC? Alipiga tano peke yake dhidi ya Buguruni United. Hakika anafaa kuitwa Ronaldo. Ronaldo hana masihara kabisa na nyavu. Anyway.

Kwanza nimemuona Ajib akifunga bao la kusawazisha kwa faulo ya moja kwa moja. Kisha nimemuona Niyonzima akiimaliza Ruvu Shooting kwa pasi yake murua iliyomfanya mmoja wa mabeki kuanguka kama mzigo wa karanga.
Mwisho nimemuona Niyonzima akimvisha kanzu beki. Ghafla nikaikumbuka ile kanzu ya Zinedine Zidane dhidi ya Ronaldo De Lima kwenye fainali ya Kombe la Dunia mwaka 2006.

Kuna vitu wanavyojaribu kuvifanya wachezaji hawa, sio vya kwenye ligi yetu kabisa. Hakika tumewahi kuwashuhudia watu wa kila kanzu miaka ya nyuma sana. Zama za kina Method Mogela na Athuman Chama ndio kipindi cha watu walipokuwa wakipigwa kanzu sio kipindi hiki cha sasa. Tuachane na hilo.

Mwishoni mwa wiki hii kuna taarifa zilizoenea kuwa Ajib amesaini Yanga. Jana, Katibu Mkuu wa Yanga, Boniface Mkwasa alitoa taarifa kuwa klabu yake haitoendelea na Niyonzima. Tukubali tu kuwa kunauwezekano mkubwa Niyonzima kutimkia Simba baada ya kuachana na Yanga. What a football?

Huu ndio mpira wa kweli. Niyonzima Simba halafu Ajib Yanga. Ni nadra sana katika ligi moja wachezaji muhimu kuondoka ndani ya msimu mmoja huku wakibadilishana timu zenye upinzani wa jadi. Hakika ni mara chache sana kwa tukio kama hili.

Katika moja ya maandiko ya mzee Arsenal Wenger aliwahi kusema kuwa “Footballers are Most Hypocrite people in the world” akiwa na maana kuwa wachezaji ni moja kati ya watu wanafiki duniani. Tuliamini kama moyo wa Niyonzima utapokea kelele za mashabiki wa Simba? Akili ya Ajibu itakubali lawama za Simba? Kila kitu acha kimalizike lakini mpira uwepo kwanza.

Hapo awali mashabiki wa Simba walimzomea Niyonzima. Yanga wakamzomea Ajib. Lakini leo kila mmoja anamkaribisha wa kwake. This is Football and that is why, Football is Fair Play Game. Naanza kuiamini FIFA ilipotueleza hilo.

Kama Torres alikubali kutoka Liverpool kwenda Chelsea. Raul Meireles pia. Ajib anaachaje. Niyonzima anaachaje? Huu ndio unafiki aliouzungumzia Wenger.
Ronaldo anamapenzi na United lakini alikwenda Real Madrid. Huwezi kuzuia pesa kwa moyo wa mapenzi. Steven Gerrard hadi leo bado anajaribu kujifariji kwa dhambi aliyoifanya mwaka 2005.

Gerrard kwenye ubora wake. Liverpool inatwaa UEFA pale Instanbul. Real Madrid, Barcelona na FC Bayern Munich zinamtaka. Alichokifanya ni kuweka mapenzi na Liverpool. Akapoteza alichoandikiwa kukipata. Anyway tuje kwenye mada muhimu.

Ajibu anakwenda kuikosa akili ya Niyonzima. Niyonzima anakwenda kuikosa miguu ya Ajibu. Najaribu kufikiria kama wawili hawa wangekuwa kwenye timu moja. Hakika hakuna zaidi ya kupigiwa mpira mwingi. Hakuna zaidi ya hicho.

Hebu jaribu kufikiria zile ‘auta’ za Ajib na chenga za Niyonzima. Umakini wa Ajib na pasi za Niyonzima. Mizungusho ya Ajib na ufundi wa Niyonzima. Ukiwa na watu hawa kwenye timu humuhitaji tena Ngoma wala Tambwe. Chirwa mmoja anakutosha.

Kuwa na watu kama Niyonzima na Ajibu kwenye timu moja. Huitaji uwepo wa Mavugo wala Blagnon. Pastory Athanas ama John Bocco tu wanakutosha. Hakika wanakutosha.

Jaribu kufikiria zile chenga za Ajibu na kanzu za Niyonzima na ule utimamu wa Chirwa wakiwa kwenye timu moja. Najaribu kuufikiria uwezo wa Mohammed Ibrahim ‘Mo’, Haruna Niyonzima na Ibrahim Ajib wakiwa kwenye timu moja. Hakika niliwahi kuomba itokee hii lakini imekuwa ngumu kidogo.

Unaachaje kujisifu unapokuwa na Ajib na Niyonzima kwenye timu yako. Uwepo wa Ajib na Niyonzima ni sawa na ule uwepo wa Zidane na Ronaldo pale Real Madrid. Chenga utapigwa na kufungwa utafungwa tu. Hakika this is football.

Watu hawa wamekosana. Vipaji vyao vimekosana. Uwepo wao pia umekosana. Katika vitu ambavyo nafikiria Ajib na Niyonzima walitakiwa kuviomba ni kuwa kwenye timu moja. Lakini imekuwa ngumu kwao.

Acha nizirudishe hizi kaseti kwenye kabati maana machozi yameshaanza kunilenga. Napomuangalia Ajib halafu Niyonzima naona ule uwepo wa Christiano Ronaldo na Wayne Rooney wakati Manchester United ikitwaa UEFA dhidi ya Chelsea.

No comments